HISTORIA ya wachezaji wa Yanga kulala mzungu wa nne imejirudia tena 
Bukoba, baada ya kulala kwa kubanana katika kitanda kimoja kama 
ilivyokuwa Mbeya, licha ya kufikia katika Hoteli ya Smart, yenye hadhi 
kubwa.
Hali kama hiyo ilijitokeza wakati timu hiyo ikijiandaa kucheza na 
Prisons, Mbeya, huku aliyekuwa Kocha Mkuu wa Yanga, Tom Saintfiet 
akianika ukweli ambao baadaye ulimponza na kufukuzwa.
Akizungumza kwa sharti la kutotajwa jina lake, mmoja wa wachezaji alisema, mambo ni yale yale kama ilivyokuwa Mbeya.
“Mambo
 kama ya Mbeya, hoteli ni nzuri, lakini wachezaji tumelala wawili wawili
 katika hoteli, pamoja na kupata huduma nzuri lakini tatizo lilikuwa ni 
hilo,” alisema mmoja wa wachezaji hao. 
Hata hivyo wachezaji 
wanatarajiwa kurejea kwa usafiri wa basi, badala ya ndege maalumu ya 
kukodi ya Kampuni ya Precision Air, iliyotumika kwenda Kagera kwa ajili 
ya mchezo huo wa Ligi Kuu Tanzania Bara, dhidi ya Kagera, uliochezwa 
jana kwenye Uwanja wa Kaitaba.
Habari zilizopatikana kutoka kwa 
kiongozi mmoja, ambaye hakutaka jina lake liandikwe gazetini, zinasema 
wachezaji hao watarejea kwa usafiri huo baada ya mchezo wao dhidi ya 
Toto African, ambao utachezwa keshokutwa Uwanja wa CCM Kirumba, Mwanza.
Wachezaji
 hao wanatarajiwa kuondoka mjini Mwanza Ijumaa, baada ya kumalizika kwa 
mchezo wao dhidi ya Toto African, kwa basi maalumu walilopewa na 
wadhamini wao, Kampuni ya Bia Tanzania TBL kupitia kinywaji chake cha 
Kilimanjaro.
Hata hivyo, gazeti hili liliweza kuongea na mkuu wa 
msafara, Mussa Katabaro, ambaye alisema anachojua yeye ni kwamba timu 
yao itarejea kwa ndege kama ilivyokuja.
Wakati huo huo, uongozi 
wa Kagera Sugar uliondoa mabango ya wadhamini wa Yanga, Kampuni ya Bia 
Tanzania, kutokana na kuwa wenyeji wa mchezo huo.
Kagera Sugar 
ambao ndio wenyeji wa uwanja huo kupitia kwa mratibu wake Mohamed 
Hussein, ilikataa katu katu mabango hayo kuwekwa katika uwanja huo, kwa 
kuwa wao ndio wa miliki wake.