
Jopo la 
Madaktari Bingwa Saba wa Hospitali ya Taifa ya Muhimbili (MNH) na 
Taasisi ya Mifupa ya hospitali hiyo (Moi), wamefanikiwa kuwatenganisha 
pacha waliokuwa wameungana kiwiliwili.Iliwalazimu mabingwa hao kutumia 
saa nne kufanikisha upasuaji huo. Mmoja wa watoto hao waliotenganishwa, 
amelazwa kwenye Wodi ya Uangalizi Maalumu (ICU) Taasisi ya Mifupa Moi 
wakati kiwiliwili kingine kilifariki.
Jopo la madaktari waliofanikisha 
upasuaji huo ni; bingwa mstaafu wa watoto ambaye aliitwa maalumu kwa 
kazi hiyo, Petronila Ngiloi, Dk Robert Mhina (mifupa) na Profesa Karim 
Manji aliyekuwa akifuatilia kwa karibu mapigo ya moyo.
 
Wengine ni Dk Karima Khalid aliyekuwa 
akiratibu dawa ya usingizi, Dk Hamis Shaaban (ubongo na uti wa mgongo), 
Dk Zaitun Bokhary (bingwa upasuaji watoto) na Dk Nyangasa (moyo na 
mishipa ya fahamu).
 
Akizungumza baada ya upasuaji huo, Dk 
Shaaban alisema walimfanyia vipimo mtoto ambaye hakuwa amekamilika na 
kugundulika kuwa hakuwa amekamilika viungo vyote achilia mbali kutokuwa 
na kichwa na macho pia hakuwa na moyo, figo, tumbo, maini ila alikuwa na
 uti wa mgongo.
 
"Uti wa mgongo ulikuwepo na ndio 
uliokuwa umeshikana na mwenzake na kuna mshipa mmoja wa fahamu ulikuwa 
unafanya kazi ndio maana alikuwa ukimgusa anachezesha mguu."
 
Alisema kinachoratibiwa kwa sasa ni 
kuangalia dawa ya usingizi aliyopewa mtoto ambaye anaendelea kupumua na 
kwamba ndani ya saa 24, dawa ya usingizi waliyomuwekea mtoto huyo 
itakuwa imeisha na ataanza kunyonya kama kawaida.
Upasuaji
 
Upasuaji
Kazi ya upasuaji huo ilianza saa mbili
 asubuhi kwa mtoto huyo wa jinsi ya kike aliyetimia kuchukuliwa vipimo 
mbalimbali ikiwemo CT Scan, MRI, Ultra sound na vingine vingi kabla ya 
upasuaji kamili kuanza saa tano asubuhi.
 
Dk Shaaban alisema ni mara ya kwanza 
kwa Moi kufanya upasuaji wa aina ile na kwamba mara nyingi wamekuwa 
wakifanya upasuaji wa watoto wanaozaliwa na vichwa vikubwa pamoja na 
mgongo wazi ambao tatizo hilo linasababishwa na upungufu wa madini ya 
folic acid.
 
Kabla ya upasuaji kuanza, mama wa 
mtoto huyo Pili Hija (24) alitumia muda wa nusu saa kufanya maombi 
maalumu ya kumwombea mtoto wake kisha kuwaruhusu madaktari kuendelea na 
upasuaji huo.
 
Akizungumza muda mfupi baada ya 
kuruhusiwa kumwona mtoto wake, Hija alisema: "Ninamshukuru Mungu kwa 
yote na nazidi kumwomba amjalie mwanangu apone kabisa, nawashukuru na 
nitazidi kuwaombea madaktari wanaomtibu mwanangu."Alijifungulia nyumbani
 Agosti 18 maeneo ya Jang'ombe, Zanzibar watoto pacha walioungana mmoja 
akiwa amekamilika viungo vyote na mwingine akiwa na kiwiliwili.

















