
 
 
Tutawatambuaje wenye mabilioni Uswisi? 
WAKATI
 Serikali na Bunge zikiwa kwenye mvutano kuhusu hatua za kufuatwa 
kurejesha mabilioni ya fedha za Kitanzania yaliyofichwa kwenye benki za 
nchini Uswisi, swali kubwa lililopo ni kwamba ni akina hasa ambao wana 
fedha huko.
Mtoaji wa hoja binafsi kuhusu suala hilo, Mbunge wa 
Kigoma Kaskazini (CHADEMA), Zitto Kabwe, amegoma kutaja majina ya vigogo
 wanaotajwa kuhifadhi fedha akitaka uchunguzi ufanyike na majina 
yafahamike wakati huo, huku serikali ikimtaka ataje majina ili ipate pa 
kuanzia kwenye uchunguzi huo.
Serikali kupitia Mwanasheria Mkuu, 
Jaji Frederick Werema, inataka kuendesha uchunguzi kuhusu madai hayo ya 
Zitto lakini kwanza inataka mbunge huyo ataje majina ya baadhi tu ya 
vigogo ambao ana ushahidi wamehifadhi fedha Uswisi.
Pamoja na 
hayo, swali moja ni lazima lipate majibu, leo au kesho. Swali lenyewe ni
 hili; ni akina nani waliokwiba fedha za Watanzania na kwenda 
kuzihifadhi ughaibuni?
Niseme mapema kwamba kuwa na akaunti nje 
ya nchi si dhambi. Dhambi inakuja pale inapofahamika kwamba fedha hizo 
zilipatikana isivyo halali.
Kwa mujibu wa ripoti ya Benki Kuu ya Uswisi iliyotolewa Juni mwaka jana, Watanzania wamehifadhi kiasi cha dola za 
 
 
Marekani 
milioni 178 (zaidi ya Sh bilioni 300) katika benki mbalimbali nchini 
humo. Ripoti hiyo haikutaja majina, wala kiwango walichonacho watu hao 
na kutokana na taratibu za kibenki za taifa hilo la Ulaya, ni lazima 
kuwepo na sababu nzito za wao kutoa taarifa zozote kuhusiana na wateja 
hao.
Hata hivyo, 
taarifa hiyo ya Benki Kuu ya Uswisi si ya kuaminika sana kwa vile taifa 
hilo linafahamika kwa kutoa taarifa zisizoaminika kuhusu kiwango hasa 
cha fedha kilichohifadhiwa na wateja wake.
Kwa
 mfano, wakati Serikali ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo ilipodai 
fedha zilizoibwa na aliyekuwa rais wa taifa hilo, Mobutu Sesesseko, 
zilizokadiriwa kufikia dola bilioni tano, Waswisi walirejesha dola 
milioni nane tu wakidai ndiyo kiasi kilichokuwapo!
Hata
 hivyo, ripoti hiyo ya Benki Kuu ya Uswisi imesaidia tu kuthibitisha 
kwamba wapo Watanzania waliohifadhi mamilioni ya dola katika akaunti 
mbalimbali nchini humo.
Swali linakuja ni akina nani hao? Nimefanya utafiti kidogo na yafuatayo yanaweza kusaidia kupata majina ya wahusika.
1. Mazingira ya wizi
Kwa
 mujibu wa ripoti ya Shirika la Kimataifa la Kupambana na Ufisadi 
(Global Financial Integrity, GFI), katika mataifa mengi ya kiafrika, 
fedha huibwa katika mazingira makubwa matatu- rushwa, ukwepaji kodi na 
mauzo ya bei za kurusha ya bidhaa au huduma mbalimbali.
Kuna
 maeneo mengine madogo kama vile ‘usafishaji’ wa fedha haramu, biashara 
ya silaha, dawa za kulevya na mambo mengine lakini GFI inaamini kwamba 
maeneo haya madogo yanafanya kazi zaidi katika mataifa ambayo yana 
serikali zisizo imara.
Kwa
 vile Tanzania ina serikali imara (walau), kulinganisha na nchi kama 
vile Somalia, sababu hizo tatu za awali kwa mujibu wa GFI ndizo 
zinazoweza kutoa picha kuhusu ni akina waliohifadhi fedha zao nchini 
Uswisi kutoka nchini mwetu.
GFI
 wametoa takwimu zinazoonyesha kuwa zaidi ya dola za Marekani milioni 
148 (Sh bilioni 246) huibwa Afrika kila mwaka kutokana na rushwa. Dola 
milioni 50 (Sh bilioni 80) kwa ukwepaji kodi na dola milioni 30 (Sh 
bilioni 48) zinazotokana na misaada kutoka kwa wahisani. Je, wapi 
tuanzie kuchunguza?
2. Idara ya Usalama wa Taifa (TISS)
Kwa
 mujibu wa gazeti la The Guardian la Tanzania la Juni mwaka jana, katika
 kipindi cha kati ya mwaka 2001 hadi 2008, Tanzania imepoteza zaidi ya 
Tsh. trilioni 1.2 kutokana na mikataba mibovu, rushwa na ununuzi wenye 
kutia shaka.
Haya 
yote yamefanyika wakati Idara ya Usalama wa Taifa nchini ikiwa inatazama
 na katika hali ya kawaida haiwezekani kwa idara hii kutofahamu chochote
 kwenye kashfa kama za ununuzi wa rada ya mtumba, Meremeta, Deep Green, 
EPA na Richmond.
Kimsingi,
 serikali imeshindwa kutoa maelezo kuhusu mradi wa dhahabu wa Meremeta 
ikidai suala hilo lina maslahi ya taifa na vigogo kadhaa wa Idara ya 
Usalama wa Taifa wanatajwa kuhusika na mradi huo.
Mwanzoni
 mwa miaka ya 2000, serikali ya Uswisi ilirejesha nchini Peru kiasi cha 
dola milioni 180 (Sh bilioni 288) zilizodaiwa kuhifadhiwa humo na 
aliyekuwa Mkuu wa Usalama wa Taifa wa nchi hiyo, Vladimiro Montesinos, 
wakati wa utawala wa Rais Alberto Fujimori.
Kwa
 vyovyote vile, watu wetu wa usalama watakuwa wanajua kitu kuhusu 
ufisadi wote huu. Ipo imani kwamba makachero wa Tanzania ni miongoni mwa
 walio bora katika Bara la Afrika. Ni lazima TISS imulikwe ili ieleze 
iwapo ilikuwa na taarifa kuhusu ufisadi uliokuwa ukifanyika lakini 
taarifa hizo hazikufanyiwa kazi na watawala au yenyewe nayo ina mkono 
kwenye hilo.
Kwa 
sababu tayari tuna ushahidi wa Montesinos. Kwa sababu tayari serikali 
imekwishakutaja usalama wa taifa kwenye ufisadi wa Meremeta.
Kuna
 uwezekano mkubwa kuwa katika hizo trilioni 1.2 zilizoibwa katika 
kipindi cha miaka kumi iliyopita, nyingine zitakuwa zimeangukia Uswisi.
3. Mawaziri
KWA
 mujibu wa taratibu zilizopo nchini, Waziri wa Fedha anaruhusiwa kutoa 
misamaha ya kodi kwa kampuni au taasisi mbalimbali pale atakapoona 
inafaa.
Tayari 
mawaziri wawili wa zamani wa serikali ya awamu ya tatu, Basil Mramba na 
Daniel Yona Ndhira, wamefikishwa mahakamani kwa kuisababishia serikali 
hasara ya Sh. bilioni 11.2 kwa kutoa msamaha wa kodi kwa kampuni ya Alex
 Stewart.
Utafiti huu
 hauna haja ya kuwatia hatiani akina Mramba lakini kwa sababu GFI 
inasema sehemu ya fedha zinazoibwa hupatikana kwa misamaha ya kodi huu 
ni mfano mmoja wapo wa namna mtu anavyoweza kutumia mamlaka yake 
kujitajirisha.
Kama 
serikali imeweza kufungua mashitaka kwa mawaziri wawili tu wa zamani wa 
fedha ambao hasara waliyotia imefikia kiasi cha Sh. bilioni 11.2, je 
imepoteza kiasi gani kwa mawaziri wengine katika awamu tofauti za 
uongozi?
Kama kweli 
serikali inataka kufahamu ni akina nani wana fedha Uswisi, sehemu nzuri 
ya kuanzia ni hapa kwa mawaziri wa fedha na uchumi waliopita kwenye 
awamu tofauti hapa nchini.
Wengi
 wa vigogo wa nchi mbalimbali waliobainika kuhifadhi fedha Uswisi 
wanatoka katika nchi zenye utajiri wa maliasili kama Tanzania.
Serikali
 inaweza kuangalia zoezi zima la ugawaji wa vitalu kwa kampuni kubwa za 
mafuta zinazotafuta uwepo wa nishati hiyo hapa nchini na misamaha 
mbalimbali iliyowahi na inayoendelea kutolewa kwa makampuni ya madini 
hapa nchini.
Kuna 
taarifa kwamba baadhi ya makampuni makubwa ya kigeni hutumia rushwa ili 
wapewe vitalu vya gesi katika maeneo ambako kuna uwezekano mkubwa wa 
kupatikana gesi kuliko mengine. Wakipewa upendeleo huo, huweka fedha 
kwenye akaunti za waliowasaidia zilizo nje ya nchi.
Uchunguzi
 wa hili usiishie tu kwa mawaziri bali uende hadi kwa makatibu wakuu wao
 na maofisa wa ngazi za juu waliokuwa na ushawishi katika utoaji wa 
misamaha, vitalu na leseni mbalimbali za uchimbaji wa madini.
Humu ndimo wanapopatikana wengi wenye fedha chafu nchini Uswisi.
4. Jeshi la Polisi Tanzania
WAKATI
 ‘dili’ zinapofanyika na kubainika, watu wa kwanza kupewa taarifa ni 
Jeshi la Polisi kwa ajili ya kukamata watuhumiwa. Hawa ndiyo wanaoandaa 
mashitaka na hawa ndiyo wataamua kuwapo au kutokuwapo kwa kesi.
Aliyewahi
 kuwa Mkuu wa Jeshi la Polisi la Afrika Kusini, Jackie Selebi, amefungwa
 jela hivi karibuni, kutokana na uhusiano wake na mhalifu maarufu nchini
 humo, Glen Agliotti. Mhalifu huyo alikuwa akimpa mkuu huyo zawadi 
mbalimbali na pia kumwekea fedha katika akaunti zake.
Tanzania
 kwa sasa ni miongoni mwa nchi zinazokamata sana dawa za kulevya ingawa 
kuna tuhuma kwamba magwiji wa biashara hizo wana mahusiano mazuri na 
baadhi ya vigogo wa Jeshi la Polisi.
Tukichunguza
 vizuri mabosi wa Polisi, tunaweza kupata kitu kuhusu akina nani 
wamehifadhi fedha zao Uswisi au popote duniani isivyo halali.
5. Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali 
KATIKA
 kashfa ya ununuzi wa rada, jina la aliyekuwa Mwanasheria Mkuu wa 
Serikali, Andrew Chenge, limeibuka mara nyingi na vyombo vya upelelezi 
vya Uingereza vinamtaja kama miongoni mwa wahusika wakuu wa kashfa hiyo.
Mwanasheria
 Mkuu wa serikali ndiye mshauri mkuu wa serikali kwenye mikataba minono 
(mikubwa) baina ya nchi na nchi au nchi na mashirika makubwa ya 
kimataifa.
Yeye ndiye
 anayeweza kuamua iwapo serikali iingie kwenye dili au la. Kama Chenge 
na baadhi ya wasaidizi wake walitajwa kwenye kashfa ya rada, ni wazi 
kwamba ofisi hii inatakiwa kumulikwa wakati serikali ikitafuta 
walioficha fedha Uswisi.
Kwa
 bahati nzuri, tayari inafahamika kuwa Chenge ana akaunti katika nchi za
 kigeni kama ilivyobainika wakati wa uchunguzi wa kashfa ya rada.
6. IKULU
Fujimori,
 Mobutu, Sani Abacha, Francosi Duvallier, Omar Bongo na Theodor Nguema 
wana mambo matatu yanayowafananisha; wote waliwahi kuwa marais katika 
nchi zao,  walifanya ufisadi wa kutisha na wote walificha mabilioni yao 
Uswisi.
Japo hii 
haimaanishi kuwa waliowahi kuwa marais wa Tanzania nao wana akaunti 
katika taifa hilo, sio vibaya kujiridhisha kwa kufanya uchunguzi ili 
kubaini kama wanaweza kuwa wameficha fedha Uswisi.
Kwa Tanzania, marais wenyewe wako wanne tu na hivyo kuchunguza si kazi ngumu.
Ikumbukwe
 kwamba rais pekee wa Tanzania kufungua ofisi ya biashara akitumia 
anuani ya Ikulu, Benjamin Mkapa, alipoumwa goti takribani miaka kumi 
iliyopita, alikwenda kutibiwa nchini Uswisi !
Labda
 tujiulize, angewezaje kuishi kule kwa miezi mitatu bila ya kuwa na 
akaunti katika mojawapo ya benki za huko? Je, ilikuw (ina) kiasi gani 
cha fedha?
Kwa mfano,
 Mkapa si ndiye aliyekuwa rais wakati wa ubinafsishaji? Serikali yake si
 ndiyo iliyopitisha misamaha mingi ya kodi kwa makampuni ya madini? Si 
mkitaka mnachunguza tu?
Tukiwa
 na nia ya kutaka kujua nani ana fedha Uswisi tutajua tu. Mimi nimetoa 
mchango wangu wenye pa kuanzia tu. Wengine wanaweza kutoa michango yao 
kwenye maeneo mengine.