LIGI KUU TANZANIA BARA 2012/2013

Michuano
 ya Ligi Kuu kuwania ubingwa wa Tanzania Bara kwa msimu wa 2012/2013 
itaanza Septemba 15 mwaka huu kwa timu zote 14 kujitupa kwenye viwanja 
tofauti.
Mechi za ufunguzi zitakuwa kati ya Simba vs African Lyon (Uwanja wa 
Taifa, Dar es Salaam), Polisi Morogoro vs Mtibwa Sugar (Jamhuri, 
Morogoro), Tanzania Prisons vs Yanga (Sokoine, Mbeya), Mgambo JKT vs 
Coastal Union (Mkwakwani, Tanga), JKT Ruvu vs Ruvu Shooting (Azam 
Complex, Dar es Salaam), Kagera Sugar vs Azam (Kaitaba, Bukoba) na Toto 
Africans vs Oljoro JKT (Kirumba, Mwanza).
Mzunguko wa kwanza 
(first round) utamalizika Novemba 11 mwaka huu ambapo kwenye mzunguko 
huo mechi ya watani wa jadi Yanga na Simba itachezwa Oktoba 3 mwaka huu 
kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
Ligi hiyo itamalizika Mei 
18 mwakani kwa mechi kati ya Toto Africans vs Ruvu Shooting (Kirumba), 
Mgambo JKT vs African Lyon (Mkwakwani), JKT Ruvu vs Mtibwa Sugar (Azam 
Complex), Tanzania Prisons vs Kagera Sugar (Sokoine), Simba vs Yanga 
(Uwanja wa Taifa), Oljoro JKT vs Azam (Sheikh Amri Abeid Kaluta) na 
Polisi Morogoro vs Coastal Union (Jamhuri).
Endapo Simba na Azam 
hazitafanikiwa kuvuka hatua mojawapo ya michuano ya Ligi ya Mabingwa 
Afrika na Kombe la Shirikisho, ratiba hiyo itafanyiwa marekebisho.
WACHEZAJI 17 WAPINGWA KWENYE USAJILI
Klabu
 mbalimbali zimewasilisha pingamizi Shirikisho la Mpira wa Miguu 
Tanzania (TFF) kupinga usajili wa wachezaji 17 walioombewa usajili 
katika timu za Ligi Kuu.
Toto Africans ya Mwanza imewawekea 
pingamizi wachezaji Enyinna Darlinton aliyeombewa usajili Kagera Sugar, 
na Mohamed Soud anayekwenda Coastal Union kwa maelezo kuwa bado ina 
mikataba na wachezaji hao.
 Pia Flamingo ya Arusha inapinga 
usajili wa wachezaji wake Kelvin Friday Iddy katika timu za Azam na 
Salim Walii (Polisi Mara) kwa vile taratibu za kuwahamisha bado 
hazijafanywa. Nayo Kagera Sugar inapinga usajili wa beki David Charles 
Luhende kwenda Yanga kwa vile ada ya uhamisho haijalipwa.
Super 
Falcon ya Chanjamjawiri, Chakechake, Pemba inapinga wachezaji wake 
wanne; Edward Christopher Shija, Samir Said Luhava (Simba), Robert 
Joseph Mkhotya (African Lyon) na Sultan Juma Shija (Coastal Union) 
kusajiliwa katika timu hizo kwa maelezo taratibu halali za uhamisho 
hazikufuatwa.
Mchezaji Othman Hassan aliyeombewa usajili Coastal 
Union anapingwa na Oljoro JKT kwa vile bado ana mkataba na timu hiyo 
unaomalizika Mei 24, 2013. Nayo Rollingstone Multipurpose Ateclass 
Foundation ya Arusha inapinga usajili wa Kigi Makassy kutoka Yanga 
kwenda Simba hadi itakapolipwa fidia ya kumlea mchezaji huyo kwa vile 
bado hajafikisha umri wa miaka 23.
 Azam inapinga usajili wa 
Ramadhan Chombo ‘Redondo’ kwenda Simba kwa maelezo bado ina mkataba naye
 unaomalizika Juni 11 mwakani. Nayo Simba inapinga Kelvin Yondani 
kusajiliwa Yanga kwa maelezo kuwa ina mkataba naye uliosainiwa Desemba 
23 mwaka jana.
 Vilevile Simba imewasilisha malalamiko ya mchezo 
usio wa kiungwana katika usajili wa Mbuyu Twite aliyeko Yanga kwa 
maelezo alisaini mkataba na klabu yao Agosti Mosi mwaka huu mbele yao, 
viongozi wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Rwanda (FERWAFA) na APR ambapo 
alilipwa dola 30,000 na nyingine 2,000 ikiwa ni fedha ya kujikimu na 
nauli yake ya kujiunga na klabu hiyo.
 Nayo Yanga inapinga Simba 
kuwaacha wachezaji Dan Mrwanda, Haruna Shamte, Kanu Mbiyavanga na Lino 
Masombo kwa maelezo walishapatiwa leseni za kucheza Ligi ya Tanzania 
walizozitumia kwenye mashindano ya Kombe la Kagame. Pia inapinga 
Ramadhan Chombo ‘Redondo’ kujiunga Simba kwa vile ana leseni ya kuchezea
 Azam kwa msimu wa 2012/2013.
Pingamizi lingine la Yanga kwa Simba
 ni kuwa imezidisha idadi ya wachezaji wa kigeni wanaotakiwa kusajiliwa 
kwa maelezo inao wanane wakati wanaoruhusiwa ni watano. Imewataja 
wachezaji hao kuwa ni Lino Masombo, Felix Sunzu, Emmanuel Okwi, Mussa 
Mude, Kanu Mbiyavanga, Pascal Ochieng, Komalmbil Keita na Daniel 
Akuffor.
Kamati ya Sheria, Maadili na Hadhi za Wachezaji ya TFF 
chini ya Mwenyekiti wake Alex Mgongolwa inatarajia kukutana Jumapili 
(Septemba 2 mwaka huu) kupitia pingamizi hizo pamoja na usajili wa 
wachezaji kwa ujumla kwa 2012/2013.